
Juzi asubuhi Wema aliandika tena katika ukurasa wake wa Instagram
kwamba yuko tayari kukabiliana na changamoto za aina zote katika safari
yake ya kuelekea bungeni.
"Nimethubutu na sitarudi nyuma, niko tayari kwa mashambulizi ya
aina yoyote," aliandika kwa kifupi mrembo huyo ambaye safari yake ya
Miss Tanzania ilianzia katika kitongoji cha Dar Indian Ocean na baadaye
Kanda ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Mrembo huyo alikisifu pia Chama Cha Mapinduzi na kuwataka wanawake
wengine wasihofie kushiriki katika kuwania nafasi mbalimbali za uongozi
pale wanapoona muda wao umefika.
Juzi, Wema aliandika kwenye ukurasa wake huo kwamba atawania ubunge
wa viti maalum kupitia CCM mkoa wa Singida katika uchaguzi mkuu ujao
utakaofanyika Oktoba mwaka huu.
Wema ambaye alifuatana na mama yake mzazi, Mariam Sepetu, aliweka
hadharani dhamira yake hiyo walipokuwa mkoani Singida mbele ya viongozi
wa chama hicho ngazi ya mkoa.
Alisema kuwa anatarajia kuchukua fomu ya kuwania nafasi hiyo ya
ubunge Julai 15, mwaka huu huku akiongeza kwamba maamuzi yake ya kuingia
kwenye ulingo wa siasa yalikuwa kwenye moyo wake na alishawahi
kumueleza marehemu baba yake (Balozi - Isack Sepetu) ambaye alimwambia
kwamba anaweza na muda ukifika asiache kujihusisha.
Aliongeza kwamba katika harakati hizo hatakubali kuona anashindwa
ingawa anafahamu wazi kuwa atakutana na changamoto mbalimbali baada ya
kuanza kwa mchakato huo.
Alisema kwamba licha ya kusoma masomo yanayohusu Biashara ya
Kimataifa badala ya siasa, marehemu baba yake hakukata tamaa na alimtaka
ajihusishe na masuala ya siasa.
Mrembo huyo ambaye pia ni msanii wa filamu za Kitanzania na
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Endless Fame ambayo kazi yake ni
kuibua wasanii na kuwasimamia kwenye tasnia hiyo, anaamini kwenye nia
hakuna kinachoshindikana.