
Naibu Waziri wa Habari, Vijana na Utamaduni, Juma Nkamia.
Wiki mbili zilizopita serikali kupitia kwa Naibu Waziri wa Habari,
Vijana na Utamaduni, Juma Nkamia, ilitangaza kusitisha matumizi mfumo
huo wa kisasa na kurudisha matumizi ya tiketi za kawaida za vishina.
Hata hivyo, katika mahojiano maalum na NIPASHE jijini Dar es Salaam
mwishoni mwa wiki, kigogo huyo wa zamani wa TFF alisema uamuzi wa
kusitisha matumizi ya ETS umelenga kurudisha ulaji wa mapato ya
milangoni kupitia mauzo ya tiketi za ziada na bandia za mfumo wa
kizamani wa vishina.
"Tiketi za elektroniki zilifuta ubebaji wa fedha za mapato kwenye
viroba. Zimekuwa chungu kwa maofisa wa TFF na Wizara ya Habari, Vijana,
Utamaduni na Michezo ambao walikuwa wameshazoea kujineemesha kwa kubeba
fedha kwenye viroba. Wizara bado haiko tayari kulipwa mgawo wa Uwanja wa
Taifa kwa hundi," kigogo huyo alisema.
Sehemu kubwa ya kasoro zilizodaiwa na TFF na serikali kuukumba
mfumo wa tiketi za elektroniki za CRDB kigogo huyo alisema ni za
kutengeneza ili kupata nafasi za kuusimamisha.
"Tiketi zitengenezwe Dar es Salaam zikauzwe Mbeya, kuna gharama
kubwa za usafirishaji na rasilimali watu. Kuna watu mfumo wa tiketi za
elektroniki unawaondoa katika ulaji wa mapato ya milangoni ndiyo maana
TFF inawakumbatia kwa kurejesha tiketi za vishina.
"Kuna baadhi ya klabu zimedai kwamba hakuna uwazi kwa maofisa wa
CRDB katika kutengeneza na kuuza tiketi, huu ni uongo mkubwa. TFF
tulipewa 'password' (namba ya siri) na CRDB inayowawezesha maofisa wa
shirikisho kuona moja kwa moja pesa inayoingia kupitia mauzo ya tiketi.
Pia kuna makubaliano ya kuonyesha idadi ya watu waliokata tiketi dakika
10 kabla ya mechi kumalizika.
"Kwa nini TFF haijatangaza tenda ya kutengeneza tiketi za kawaida
licha ya serikali kusitisha matumizi ya tiketi za elektroniki? Nani
anayetengeneza tiketi kwa sasa? Huu uvunjaji wa katiba ya shirikisho.
"Ni aibu kutoka kwenye mfumo wa kisasa wenye manufaa na kurudi
kwenye mfumo wa kizamani ambako nchi nyingi zimeshauacha," kigogo huyo
alisema zaidi huku akishauri TFF, serikali na klabu zitafute mbinu
nyingine za kupata fedha mbali na mapato ya milangoni.
"Angalia viwango vya wachezaji kina (Emmanuel) Okwi, (Ibrahim)
Ajibu wa Simba, (Simon) Msuva, (Mrisho) Ngasa wa Yanga. Je, klabu zao
zinatumia fursa hiyo katika kutengeneza jezi zenye majina ya wachezaji
hao na kuuza kwa mashabiki?" Alihoji kigogo huyo.
"Viongozi wetu wa soka kwa sasa wanafikiria kuhusu mapato ya
milangoni tu badala ya kuja na mikakati mingine ya kuinua uchumi na soka
la Tanzania. Waangalie haki za matangazo ya televisheni. Tuna Simba TV
ndani ya Azam TV wanaodhamini ligi kuu, tunapaswa kuwa na Yanga TV,
Mbeya City TV, TFF TV ndani ya Azam TV.
"Viongozi wetu wa soka wamefumbia macho mambo ya maendeleo huku
wakiweka nguvu nyingi kupiga vita tiketi za elektroniki zinazozuia wizi
wa mapato ya milangoni."
CHANZO:
NIPASHE