watu walio tembelea leo

Kigogo TFF aanika madudu tiketi elektroniki.


Naibu Waziri wa Habari, Vijana na Utamaduni, Juma Nkamia.
Wakati serikali ikitangaza kusitisha matumizi ya mfumo wa tiketi za elektroniki (ETS) kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, mmoja wa waliokuwa viongozi wa juu katika utawala uliopita wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), ameanika 'madudu' ya ulaji wa watendaji wa shirikisho na serikali kupitia matumizi ya tiketi za vishina.
 
Wiki mbili zilizopita serikali kupitia kwa Naibu Waziri wa Habari, Vijana na Utamaduni, Juma Nkamia, ilitangaza kusitisha matumizi mfumo huo wa kisasa na kurudisha matumizi ya tiketi za kawaida za vishina.
 
Hata hivyo, katika mahojiano maalum na NIPASHE jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, kigogo huyo wa zamani wa TFF alisema uamuzi wa kusitisha matumizi ya ETS umelenga kurudisha ulaji wa mapato ya milangoni kupitia mauzo ya tiketi za ziada na bandia za mfumo wa kizamani wa vishina.
 
"Tiketi za elektroniki zilifuta ubebaji wa fedha za mapato kwenye viroba. Zimekuwa chungu kwa maofisa wa TFF na Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ambao walikuwa wameshazoea kujineemesha kwa kubeba fedha kwenye viroba. Wizara bado haiko tayari kulipwa mgawo wa Uwanja wa Taifa kwa hundi," kigogo huyo alisema.
 
Sehemu kubwa ya kasoro zilizodaiwa na TFF na serikali kuukumba mfumo wa tiketi za elektroniki za CRDB kigogo huyo alisema ni za kutengeneza ili kupata nafasi za kuusimamisha.
 
"Tiketi zitengenezwe Dar es Salaam zikauzwe Mbeya, kuna gharama kubwa za usafirishaji na rasilimali watu. Kuna watu mfumo wa tiketi za elektroniki unawaondoa katika ulaji wa mapato ya milangoni ndiyo maana TFF inawakumbatia kwa kurejesha tiketi za vishina.
 
"Kuna baadhi ya klabu zimedai kwamba hakuna uwazi kwa maofisa wa CRDB katika kutengeneza na kuuza tiketi, huu ni uongo mkubwa. TFF tulipewa 'password' (namba ya siri) na CRDB inayowawezesha maofisa wa shirikisho kuona moja kwa moja pesa inayoingia kupitia mauzo ya tiketi. Pia kuna makubaliano ya kuonyesha idadi ya watu waliokata tiketi dakika 10 kabla ya mechi kumalizika.
 
"Kwa nini TFF haijatangaza tenda ya kutengeneza tiketi za kawaida licha ya serikali kusitisha matumizi ya tiketi za elektroniki? Nani anayetengeneza tiketi kwa sasa? Huu uvunjaji wa katiba ya shirikisho.
 
"Ni aibu kutoka kwenye mfumo wa kisasa wenye manufaa na kurudi kwenye mfumo wa kizamani ambako nchi nyingi zimeshauacha," kigogo huyo alisema zaidi huku akishauri TFF, serikali na klabu zitafute mbinu nyingine za kupata fedha mbali na mapato ya milangoni.
 
"Angalia viwango vya wachezaji kina (Emmanuel) Okwi, (Ibrahim) Ajibu wa Simba, (Simon) Msuva, (Mrisho) Ngasa wa Yanga. Je, klabu zao zinatumia fursa hiyo katika kutengeneza jezi zenye majina ya wachezaji hao na kuuza kwa mashabiki?" Alihoji kigogo huyo.
 
"Viongozi wetu wa soka kwa sasa wanafikiria kuhusu mapato ya milangoni tu badala ya kuja na mikakati mingine ya kuinua uchumi na soka la Tanzania. Waangalie haki za matangazo ya televisheni. Tuna Simba TV ndani ya Azam TV wanaodhamini ligi kuu, tunapaswa kuwa na Yanga TV, Mbeya City TV, TFF TV ndani ya Azam TV.
 
"Viongozi wetu wa soka wamefumbia macho mambo ya maendeleo huku wakiweka nguvu nyingi kupiga vita tiketi za elektroniki zinazozuia wizi wa mapato ya milangoni."
 
CHANZO: NIPASHE